Wednesday, June 1, 2016



Kiongozi na muasisi wa chama cha ukombozi wa Sahara ya Magharibi-Polisario, Mohammed Abdelaziz amefariki dunia baada ya maradhi ya muda mrefu. Habari hizo zimetangazwa na chama cha ukombozi wa Sahara ya Magharibi kilichosema marehemu alikuwa na zaidi ya miaka 60. Chama cha Polisario kimetangaza siku 40 za maombolezi na kusema katibu mkuu mpya atateuliwa kipindi hicho kitakapomalizika. Rais Abdelaziz Bouteflika wa Algeria ametangaza pia wiki moja ya maombolezi nchini mwake. Itafaa kusema hapa kwamba makao makuu ya chama cha ukombozi wa Sahara ya magharibi-Polisairio yanakutikana katika mji wa kusini mwa Algeria,Tindouf. Kifo cha Mohammed Abdelaziz aliyekiongoza chama cha Polisario kwa miongo minne, kimejiri katika wakati ambapo mvutano unazidi makali kuhusu hatima ya eneo la Sahara ya Magharibi. Polisario wamekuwa kwa miongo minne sasa wakipigania uhuru wa eneo hilo kubwa na tajiri kwa madini lililoko katika mwambao wa bahari ya Atlantik. Moroko imelivaamia eneo hilo baada ya mkoloni wa zamani Uhispania kuondoka mwaka 1975.

No comments:

Post a Comment