Wednesday, December 9, 2015

Jeshi la Uingereza kufanya mazoezi Kenya



Uingereza imetia saini mkataba wa makubaliano ya kuendelea kuwa na kambi yake ya majeshi nchini Kenya kwa muda wa miaka mitano zaidi.
Mkataba huo mpya umeiruhusu Kenya kuwashtaki na kuwafunga wanajeshi wa Uingereza wanaovunja sheria za nchi hiyo ya Afrika Mashariki.
Swala hilo la kuwachukulia hatua wanajeshi wa Uingereza lilitishia kuvunja uhusiano baina ya nchi hizo mbili.
Baada ya majadiliano makali Uingereza umekubali wanajeshi wake wanaovunja sheria wakiwa nchini Kenya kushitakiwa.

Awali walikuwa wanaondoshwa nchini Kenya na kurejea makwao huku waliotendewa uovu wakisalia pasi na njia ya kutafuta haki.
Kipengee hicho kilichelewesha makubaliano ya kuyaongezea muda majeshi ya Uingereza.
Maafisa wa Uingereza watawahukumu wanajeshi wanaovunja sharia wakiwa kazini, lakini shughuli hiyo itafanyika Kenya.
Baadhi ya wanajeshi wa Uingereza walio nchini Kenya wameshutumiwa kwa uhalifu kama ubakaji, mauaji na kuwahepa wanawake baada ya kuwatia mimba.
Hata hivyo serikali ya Uingereza imekana kuwatetea wanajeshi kama hao na kuzuia wasichukuliwe hatua za kisheria.

Wanajeshi 10,000 wa Uingereza hufanya mazoezi nchini Kenya kila mwaka.
Kenya pia hutuma wanajeshi wake Uingereza kwa masomo ya juu.
Mwaka jana Uingereza ilitumia karibu $90,000 nchini Kenya, huku asilimia kubwa ya fedha kutoka Uingereza zikiingia moja kwa moja kwenye uchumi wa taifa hilo.
Balozi wa Uingereza nchini Kenya Nicholas Hailey amesema nchi hiyo inapania kujenga makao makuu mapya Nairobi kwa gharama ya dola milioni $20.
Mkataba huu mpya sharti uratibiwe na bunge za mataifa hayo mawili.
Mkataba uliopo utamalizika mwezi Aprili mwakani.

No comments:

Post a Comment