Wednesday, December 30, 2015


Serikali nchini Ubelgiji imefuta sherehe na shamrashamra za Mwaka Mpya pamoja na ufyatuaji wa fataki kwenye mji mkuu wa nchi hiyo, Brussels, baada ya kugundulika njama ya wanamgambo wa itikadi kali kutaka kufanya mashambulizi wakati wa sikukuu hiyo. Meya wa Brussels, Yvan Mayeuer, amesema kwa bahati mbaya wamelazimika kufuta sherehe hizo zilizopangwa kufanyika leo usiku. Mji wa Brussels wenye wakaazi milioni 1.2 umekuwa katika hali ya tahadhari tangu Ufaransa iliposema watu kadhaa waliohusika na mashambulizi ya kigaidi ya Paris, Novemba 13, wanaishi mjini Brussels, ambako ni makao makuu ya Umoja wa Ulaya na Jumuia ya Kujihami ya NATO. Siku ya Jumanne polisi walisema wamewakamata watu wawili wanaotuhumiwa kupanga mashambulizi wakati wa sikukuu ya Mwaka Mpya mjini Brussels. Waziri Mkuu wa Ubelgiji, Charles Michel amesema uamuzi wa kufutwa sherehe za Mwaka Mpya ulikuwa mgumu, lakini ulio sahihi.

No comments:

Post a Comment