Tuesday, November 10, 2015

Mwanahabari aliyekamatwa Kenya aachiliwa

John Ngirachu Facebook 

Bw Ngirachu alikamatwa akiwa katika majengo ya Bunge
Mwanahabari mmoja mashuhuri nchini Kenya aliyekuwa amekamatwa na kuzuiliwa na maafisa wa usalama Kenya baada ya kudaiwa kuchapisha habari kuhusu tuhuma za ufisadi serikalini ameachiliwa huru.
Mwanahabari huyo John Ngirachu wa shirika la habari la Nation Media Group ameachiliwa baada ya kuandikisha taarifa na maafisa wa uchunguzi wa jinai akiwa ameandamana na mawakili wake wawili.
Bw Ngirachu, ambaye ni mhariri anayeangazia habari za bunge, anadaiwa kuandika taarifa iliyonukuu habari kutoka kwa kikao cha faraghani cha Kamati ya Bunge kwenye gazeti la Daily Nation.
Habari hizo zinahusu ufisadi katika Wizara ya Usalama na Masuala ya Ndani kuhusu matumizi ya Sh3.5 bilioni pesa za Kenya.
Waziri wa usalama wa ndani Joseph Nkaissery, anasema aliwasilisha habari hizo faraghani na anasema yeyote aliyefichua habari hizo sharti aeleze alizitoa wapi.
“Kama waziri anayesimamia usalama, nachukulia hatua hii kama njama ya kudhuru taifa, kuhujumu juhudi za kudumisha usalama na kuonyesha wizara hii kama fisadi na isiyofuata sheria.
"Haikubaliki,” alisema Nkaissery kwenye kikao na wanahabari siku moja baada ya kuchapishwa kwa habari hizo.
Lakini mmoja wa wahariri wakuu wa shirika la habari la Nation Media, Linus Kaikai amekanusha madai hayo
“Hatujakiuka maadili yoyote, vikao vya bungeni wazi na katika katiba tunaruhusiwa kuwa katika vikao vile’’.
"Habari hizo zilijulikana Nkaissery alipofika katika kikao hicho cha kamati ya bunge,” Bw Linus Kaikai ameiambia BBC.
“Kwa sasa mawakili wetu wanashughulika kujaribu kumtoa korokoroni’’.
‘’Kwa sasa kile tunajali zaidi ni uhuru wa Ngirachu.”
Bw Ngirachu, aliandika mara ya kwanza kwenye mtandao wake wa Twitter Novemba 5 akidai kuandamwa na afisa wa uchungzi wa jinai aliyemtaka "aeleze alikotoa habari hizo”.
"Afisa wa CID anapigia simu wanahabari wote walioandika kuhusu maswali ya Mkaguzi Mkuu wa hesabu za Serikali kuhusu matumizi ya Sh3.8 bilioni katika wizara ya masuala ya ndani,” aliandika.
Kwa mujibu wa Bw Ngirachu, habari hizo zilitolewa kwenye kikao cha Kamati ya Uhasibu Bungeni (PAC).
Watumiaji wa mtandao wa Twitter wamekuwa wakieleza kukasirishwa kwao na kukamatwa kwa mwanahabari huo, wakitumia kitambulisha mada #FreeNgirachu, yaani mwachilie huru Ngirachu.
Kiongozi wa Muungano wa upinzani CORD Raila Odinga pia ametoa taarifa akishutumu kukamatwa kwa mwanahabari huyo na kuitaka serikali imwachilie huru mara moja.
Waandishi wa habari wanapanga kuandamana hapo kesho ili kupinga kukamatwa kwake na kuishinikiza serikali kumuachilia huru.
Aidha shirika la wanahabari wanapanga kuwasilisha kesi mahakamani ya kutaka aachiliwe huru.

No comments:

Post a Comment